<?xml version="1.0" encoding="UTF-8"?>
<rdf:RDF xmlns="http://purl.org/rss/1.0/" xmlns:rdf="http://www.w3.org/1999/02/22-rdf-syntax-ns#" xmlns:dc="http://purl.org/dc/elements/1.1/">
<channel rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/809">
<title>Kiswahili &amp; Other African Languages</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/809</link>
<description/>
<items>
<rdf:Seq>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6402"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6306"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6275"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6015"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5908"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5218"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5211"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1127"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1125"/>
<rdf:li rdf:resource="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1114"/>
</rdf:Seq>
</items>
<dc:date>2026-05-15T12:31:52Z</dc:date>
</channel>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6402">
<title>Jalada kama mtindo wa kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano na Chozi la heri</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6402</link>
<description>Jalada kama mtindo wa kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano na Chozi la heri
ONG’ALE, Any'ayi Phillis
Upekee katika uundaji wa kazi ya fasihi huitwa mtindo na hutofautiana kutoka mwandishi mmoja hadi mwingine. Mtunzi huweza kuchagua mtindo wa kueleza kazi yake unaodhihirika sio tu ndani mwa kazi hiyo bali pia kupitia jalada la kitabu kama vile jalada la mbele na la nyuma. Kimsingi, jalada huwa na mawasilisho kama vile rangi na picha zinazowasilisha maudhui yaliyomo katika kazi husika ya fasihi. Wahakiki wengi wana mazoea ya kuchambua majalada hayo kwa kutaja tu rangi na picha zinazodhihirika na kuzihusisha na matukio yaliyomo kitabuni moja kwa moja bila kuzingatia nadharia yoyote. Wengine huzingatia jalada la mbele tu katika uchambuzi wao na kupuuza lile la nyuma lililo na blabu iliyo na mtindo wake wa kimuundo na kiisimu. Utafiti huu ulifanywa kwa lengo kuu la kuchunguza matumizi ya jalada kama mtindo katika kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014). Utafiti uliongozwa na madhumuni matatu; kubainisha rangi na picha katika majalada kama mtindo wa kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014), kuchambua maudhui yanayowasilishwa na rangi na picha katika majalada kama mtindo wa kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014) na kuhakiki vipashio vinavyojenga blabu kama mtindo wa kuakisi maudhui katika riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014). Utafiti uliongozwa na nadharia ya Semiotiki kwa mujibu wa Peirce na kuendelezwa na Ferdinand, Barthes, Wamitila na Massamba, na pia nadharia ya Muundo Kipera kwa mujibu wa Swales. Kimsingi Semiotiki hutazama ishara za matini zinavyofungamanishwa na maana kifasihi. Nadharia hii ilitumiwa kuchambua namna rangi na picha zilizopo kwenye majalada zinavyoingiliana na matukio katika riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014). Nadharia ya Muundo Kipera hushughulika na vipashio vinavyopatikana katika uandishi wa blabu, ikiwemo hatua za uandishi na mshikamano. Utafiti ulizingatia muundo kiuchanganuzi. Eneo la utafiti lilikuwa la kithematiki ya umitindo na kiisimu katika fasihi. Usampulishaji maksudi ulitumika ambapo sampuli mbili, riwaya ya Utengano (Mohammed, 2009) na Chozi La Heri (Matei, 2014) ziliteuliwa. Data kutoka kwenye riwaya ilikusanywa kupitia mbinu ya unukuzi. Orodha ya uhakiki ilitumika kama kifaa. Uchanganuzi wa data ulifanywa kimaudhui na kuwasilishwa kwa maelezo ya kinathari. Matokeo ya utafiti yalibainisha rangi kama vile nyeupe, nyeusi, nyekundu, kijani kibichi, manjano, samawati na hudhurungi. Picha zilizobainishwa katika Utengano (Mohammed, 2009) ni kama vile mwanamke aliyevalia buibui, kasri, bahari na nyumba ya matope na mabati. Katika Chozi la Heri (Matei, 2014) kuna picha ya jicho linalodondoka chozi ambamo kuna vijana watatu wanaoukumbatiana. Maudhui kutokana na rangi na picha ni kama vile ukahaba, ufisadi, ukoloni mamboleo, utengano, mapenzi, ndoa na nafasi ya mwanamke. Aidha, matokeo yalidhihirisha misogeo hatua minne ya uandishi wa blabu katika riwaya zote mbili; maelezo au utangulizi, kuhusu mwandishi, kampuni ya uchapishaji na maudhui kutoka kitabuni. Maudhui kutokana na misogeo hatua ni utengano, mabadiliko, tamaa na ukabila. Vipengele vya mshikamano kama vile urejeshi, uunganishaji, udondoshaji ubadilishaji na hiponimu vilibainishwa. Utafiti huu utasaidia katika uchambuzi wa majalada ya kazi mbalimbali za fasihi ya Kiswahili kinadharia. Aidha, utasaidia wahakiki wa fasihi, wakuza mitaala na kampuni za uchapishaji kuzingatia zaidi uboreshaji wa majalada ili kuvutia makini ya wasomaji.
Master's Thesis
</description>
<dc:date>2025-11-11T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6306">
<title>Vipengele vya fasihi vinavyojenga taswira ya mwanamke katika vitabu teule vya Biblia takatifu</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6306</link>
<description>Vipengele vya fasihi vinavyojenga taswira ya mwanamke katika vitabu teule vya Biblia takatifu
ANGWEHE, Aglen
Lugha ni chombo cha kipekee kinachofinyangwa kuwasilisha taswira ya masuala changamano katika jamii. Lugha inapofinyangwa huzua fasihi, ambayo ni kioo cha jamii. Biblia Takatifu ni kitabu mojawapo kikongwe cha fasihi ambacho mafunzo yake hurejelewa na zaidi ya watu bilioni 2.4. Katika Biblia Takatifu, kitabu cha Mwanzo 1:26-27, lugha inatuchorea taswira kuhusu hadhi sawa ya mwanamke na mwanamume kulingana na mpango asili wa Mungu. Hata hivyo, katika hiyo hiyo Biblia Takatifu tunakumbana na taswira changamano kumhusu mwanamke. Utafiti huu ulichanganua vipengele vya fasihi vinavyojenga taswira ya mwanamke katika vitabu teule vya Biblia Takatifu. Madhumuni mahsusi ni: kubainisha maumbo ya fasihi yanayojenga taswira ya mwanamke katika Biblia Takatifu, kupambanua mitindo ya lugha inayojitokeza katika maumbo ya fasihi yanayojenga taswira ya mwanamke katika Biblia Takatifu na kuchanganua maudhui yanayojitokeza katika maumbo na mitindo ya lugha inayojenga taswira ya mwanamke katika vitabu teule vya Biblia Takatifu. Utafiti ulizingatia kiunzi cha nadharia chenye mihimili kutoka nadharia tatu; nadharia ya Umaumbo iliyoasisiwa na Shlovsky (1904) na kuendelezwa na Maryanne (1999); Umuundo mpya iliyoasisiwa na Derrida (1972) na kuendelezwa na Crick (2016) na Ufeministi huru kwa mujibu wa Wamitila (2003) iliyoasisiwa na Bouchier (1983). Mihimili ya nadharia ya umaumbo kuwa kazi yoyote katika fasihi ina sifa teule kisanii zinazomwongoza anayetafiti. Pili, kwa sababu fasihi inajumlisha lugha, lugha ni mhimili katika sayansi ya fasihi. Tatu, fasihi haiwezi kutengwa na jinsi inavyowasilishwa kwani umbo la kazi huirembesha na pia ni sehemu ya yaliyomo. Mihimili ya nadharia ya Umuundo mpya iliyotumiwa n maana huumbwa kwenye lugha na lugha ni mhimili mkuu katika kuchanganua maswala katika jamii. Mhimili wa nadharia ya ufeministi huru uliotumiwa ni ule unaomuongoza mhakiki kushambulia yaliyoandikwa na namna wanavyowasilisha wahusika wanawake. Utafiti ulizingatia muundo wa kiuchanganuzi. Idadi lengwa ilikuwa vitabu 66 vya Biblia Takatifu. Kwa kuzingatia madhumuni ya utafiti usampulishaji dhamirifu ulifanywa kufikia kiwango ambacho hakuna data nyingine mpya ilipatikana. Vitabu 12 vilisampuliwa; Mwanzo, Waamuzi, Ruthu, Wafalme 1 na 11, Esta, Methali, Wimbo ulio Bora na Luka Mtakatifu, Matayo, Samweli I na II. Orodhahakiki ilitumiwa kudondoa data ya maumbo, mitindo na maudhui yanayojenga taswira ya mwanamke katika Biblia Takatifu. Data ilipangwa na kuwasilishwa kimaelezo. Matokeo yalibaisha kuwa maumbo ya fasihi yanayojenga taswira ya mwanamke katika Biblia Takatifu huwasilishwa kwa mitindo teule ya lugha inayodhihirisha maudhui yanayojenga taswira hasi au chanya kumhusu mwanamke. Utafiti unatarajiwa kuwafahamisha wanajamii kuwa fasihi ni namna ya kipekee ya kutumia lugha kujenga taswira ya maswala changamano katika jamii.
Mater's Thesis
</description>
<dc:date>2024-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6275">
<title>Uchanganuzi kimofosemantiki wa anthroponimu za Kimaragoli zinazojengwa na nomino za kawaida za Kiswahili</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6275</link>
<description>Uchanganuzi kimofosemantiki wa anthroponimu za Kimaragoli zinazojengwa na nomino za kawaida za Kiswahili
ODARI, Morris Salano
Maana za maneno zinaweza kubadilika kulingana na muktadha wa ufasiri, hali inayoweza kutinga uwasilishaji wa maana ikusudiwayo. Mabadiliko ya kimaana kama haya yanadhihirika pia katika uchunguzi wa anthroponimu za Kimaragoli. Ingawa tafiti zimefanywa kuhusu maana kileksika za anthroponimu za Kimaragoli, vyanzo vya anthroponimu hizo kutokana na nomino za kawaida za Kiswahili, mbinu za kimofolojia zinazounda anthroponimu hizo, pamoja na mabadiliko yake kimaana hazijashughulikiwa. Kutokana na msingi huu, utafiti huu ulichanganua kimofosemantiki anthroponimu za Kimaragoli zilizoundwa kutokana na nomino za kawaida za Kiswahili. Utafiti huu uliongozwa na madhumuni yafuatayo: kuainisha nomino za kawaida za Kiswahili zijengazo anthroponimu za Kimaragoli katika vikoa maana; kufafanua mabadiliko ya kisemantiki katika anthroponimu za Kimaragoli zijengwazo kwa nomino za kawaida za Kiswahili; na kuchanganua mbinu za kimofolojia za uundaji wa anthroponimu za Kimaragoli zijengwazo kwa nomino za kawaida za Kiswahili. Uchunguzi huu uliongozwa na Nadharia ya Pragmatiki Leksia iliyoasisiwa na Blutner (1990). Nadharia hii huchunguza maana ya leksimu kipragmatiki. Kwa kuzingatia muundo wa kimaelezo, utafiti ulifanyika maktabani na nyanjani katika gatuzi Dogo la Sabatia, kaunti ya Vihiga. Usampulishaji dhamirifu ulitumiwa kuteua nomino za kawaida za Kiswahili, watafitiwa, hospitali pamoja na eneo la utafiti. Data ya anthroponimu za Kimaragoli ilikusanywa kutoka kwa baraza la wazee la Wamaragoli pamoja na sajili za majina katika hospitali teule. Data ya utafiti ilikusanywa kwa kutumia mbinu za upekuzi maktabani na usaili usorasmi, na vifaa vya utafiti vilijumuisha orodhahakiki na mwongozo wa usaili. Uhalali, ukubalifu na utegemezi wa data ulithibitishwa na wataalamu wa lugha na jamii ya Wamaragoli. Maadili ya utafiti yalizingatiwa kabla, wakati na baada ya utafiti kwa mujibu wa matakwa ya kibali cha utafiti kutoka MUERC na NACOSTI. Data ilichanganuliwa kimaudhui na kuwasilishwa kimaelezo na katika majedwali. Matokeo ya utafiti yamedhihirisha kuwa nomino za kawaida za Kiswahili zinaweza kuainishwa katika vikoa maana vya wanyama, ndege, vifaa, na mimea. Mabadiliko ya kimaana katika anthroponimu za Kimaragoli zilizojengwa kwa nomino za kawaida za Kiswahili hujumuisha upanuzi, kisio na ubanaji wa maana. Aidha, anthroponimu za Kimaragoli zijengwazo kutokana na nomino za kawaida za Kiswahili huzingatia mbinu za kimofolojia kama vile ukopaji, uhusishaji, uradidi, mwambatanisho na uhulutishaji. Utafiti ulipendekeza tafiti zaidi zifanywe kuhusu mchango wa aina nyingine za nomino pamoja na kategoria zingine za maneno katika ujenzi wa anthroponimu za Kimaragoli na lugha nyinginezo. Matokeo ya utafiti huu yanachangia mijadala ya dhima ya Kiswahili katika kuendeleza misamiati ya lugha nyingine za kiasili, maarifa ya semantiki, mofolojia na onomastiki. Aidha, utafiti huu ni kanzi inayoelimisha kuhusu anthroponimu za Kimaragoli, mabadiliko ya kimaana katika anthroponimu hizo na pia mbinu za kimofolojia zinazozijenga kutokana na nomino za kawaida za Kiswahili.
Master's Thesis
</description>
<dc:date>2024-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6015">
<title>Mchango wa Ushairi wa Kiganda katika kuendeleza umitindo wa Ushairi wa Kiswahili: Mfano wa ufundishaji wa ushairi katika wilaya ya Mukono-nchini Uganda</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/6015</link>
<description>Mchango wa Ushairi wa Kiganda katika kuendeleza umitindo wa Ushairi wa Kiswahili: Mfano wa ufundishaji wa ushairi katika wilaya ya Mukono-nchini Uganda
ATUKUNDA, Edwine
Wanafunzi wengi nchini Uganda wanachukulia utanzu wa ushairi wa Kiswahili kuwa mgumu na wanapata ugumu huo katika kujifunza ushairi wa Kiswahili.Ugumu katika ujifunzaji wa ushairi wa Kiswahili umesababisha matokeo mabaya katika mtihani wa kitaifa katika somo la ushairi wa Kiswahili nchini Uganda.Hata hivyo ushairi wa Kiganda umekuwa unafanywa vizuri katika mtihani wa kitaifa. Wanafunzi hawa wanasomea katika mandhari sawa, utafiti huu ulichunguza kwa nini wanafunzi wanaofanya mtihani wa ushairi wa Kiganda wanatenda vizuri kuliko wanafunzi wa ushairi wa Kiswahili. Kwa hivyo utafiti huu ulichanganua mchango wa ushairi wa Kiganda katika kuendeleza umitindo wa ushairi wa Kiswahili, mfano wa ufundishaji wa ushairi katika wilaya ya mukono-nchini Uganda.Madhumuni ya utafiti huu yalikuwa: Kufafanua jinsi muundo wa ushairi wa Kiganda unavyoweza kuendeleza muundo wa ushairi wa Kiswahili kupitia ufunzaji na ujifunzaji.Kudadavua jinsi ushairi wa Kiganda unaweza kusahilisha mtindo katika ushairi wa Kiswahili kupitia ufunzaji na ujifunzaji na kutathimini jinsi ushairi wa Kiganda unaweza kukuza maudhui katika ushairi wa Kiswahili kupitia ufunzaji na ujifunzaji. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya umitindo yaViktor Shklovsky (1904) na kuelezwa na Mbatia (2001) katika muktadha wa Kiswahili na umuundo ambayo iliasisiwa na Ferdinard de Saussure (1909) na Ntarangwi (2004), mihimili ya nadharia hii ni: Fasihi inastahili kuchunguzwa kama muundo mmoja uliojengwa kwa vipengele tofauti vinavyoshirikiana kukiunda kitu kizima. Pili huchunguza vipengele mbalimbali vya mfumo wa fasihi kwa kuchunguza jinsi vinavyohusiana na kuchangiana katika kukamilisha kazi husika. Tatu hulenga maana katika matini ya kifasihi na kupuuza maswala mengine ya nje kama muktadha. Utafiti huu ulitumia muundo elezi na data za utafiti huu zilichambuliwa kithamano. Mashairi yalikusanywa kutoka diwani mbili za Kiswahili na mbili za Kiganda. Mashairi 60 yalikusanywa yaani 30 ya Kiganda na 30 ya Kiswahili na 15 yalichaguliwa kutoka kila lugha kwa kutumia uteuzi nasibu. Mashairi yalitolewa kwenye diwani za Kiswahili; Malenga wa ziwa kuu ya Wallah bin Wallah naSauti ya dhikiya Abdilatif Abdalla na za Kiganda; Ab’Oluganda ab’Enda emu ya Hugo Sematimbana Balya n’ensekeezi ya Masagazi K. Vilichaguliwa kwa kuwa viko kwenye silabasi. Kundi lengwa ni Walimu watano wa Kiganda na watano wa Kiswahili ambao walichaguliwa kimakusudi na kushiriki katika uchambuzi ambao uliandamana na maoni yao kuhusu ujifunzaji na ufunzaji wa ushairi. Mashairi yalianishwa na ya Kiganda yalitafsiriwa kwa Kiswahili. Data ilikusanywa kwa kutumia simu kunasa sauti. Mashairi yalinukuliwa, yalitafsiriwa, na kisha kuchambuliwa kimuundo, kimtindo na kimaudhui. Data za utafiti huu ziliwasilishwa kwa mfumo wa kinathari.  Utafiti huu ulikuwa utafiti wa nyanjani na maktabani, ulifanyiwa katika wilaya ya Mukono. Shule tano zilitumiwa kati ya shule ishirini zinazofunza Kiswahili, ziliteuliwa kimakusudi kwa kuwa zinafundisha Kiswahili na Kiganda kwenye kiwango cha A kisha uchanganuzi wa data ulifanywa kithamano na data kuwasilishwa kwa mjadala. Utafiti huu uligundua kuwa ushairi wa Kiswahili waweza kukopa vipengele vya muundo, mtindo, na maudhui vya ushairi wa Kiganda na kuviendeleza vipengele hivi katika ushairi wa Kiswahili. Utafiti huu ulifafanua jinsi mwalimu wa ushairi wa Kiswahili anavyoweza kuhamisha maarifa kutoka ushairi wa Kiganda hadi wa Kiswahili. Utasaidia kuendeleza ushairi wa Kiswahili kuhamisha maarifa ya ujifunzaji na ufunzaji kutokana na ushairi wa Kiganda ili kusahilisha ujifunzaji wa ushairi wa Kiswahili na kuuendeleza.
PhD Thesis
</description>
<dc:date>2023-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5908">
<title>Mikakati na mitindo katika ujifunzaji wa kiswahili kama lugha ya biashara miongoni mwa wafanyabiashara jijini Kampala-Uganda</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5908</link>
<description>Mikakati na mitindo katika ujifunzaji wa kiswahili kama lugha ya biashara miongoni mwa wafanyabiashara jijini Kampala-Uganda
MUTENYO, Aidah
Dhima mojawapo ya lugha ya Kiswahili ni ukuzaji wa sekta ya uchumi. Kiswahili kama lugha ya pili nchini Uganda, kilianzishwa kwa ajili ya kuendeleza biashara na dini. Ujifunzaji na matumizi yake hayajaendelezwa kwa kina. Hata hivyo unapokwenda katika maeneo ya biashara, utakuta Kiswahili kikitumika miongoni mwa wafanyabiashara. Hali ya jinsi wanavyojifunza na kutumia Kiswahili kuendeleza biashara na changamoto wanazokumbana nazo katika matumizi ndilo pengo lililoshughulikiwa katika utafiti huu. Azma ya utafiti huu ilikuwa kuchunguza mikakati na mitindo katika ujifunzaji wa Kiswahili kama lugha ya biashara miongoni mwa wafanyabiashara jijini Kampala, Uganda. Madhumuni mahsusi yalikuwa: Kufafanua mikakati na mitindo ya kujifunza Kiswahili kama lugha ya kibiashara jijini Kampala Uganda, kutathmini jinsi mikakati na mitindo mbalimbali huwezesha kujifunza Kiswahili kama lugha ya  kibiashara jijini Kampala na kupambanua  changamoto zinazokumba wafanyabiashara wakati wa kujifunza Kiswahili kibiashara na kuchanganua mikakati ya namna ya kutatua changamoto zinazowakabidhi wafanyabiashara kujifunza Kiswahili kibiashara. Utafiti huu uliongozwa na kiunzi cha nadharia mbili: Kwanza, Nadharia ya Stephen Krashen (1987) ambayo ina mihimili mitano; nadharia tete ya upataji/ujifunzaji, nadharia tete ya mfumo asili, nadharia tete ya dhana mpya na nadharia tete ya kichujio athari. Pili, Nadharia ya  modeli ya elimu ya  Richard Gardener (2000). Mihimili iliyohusika ni; mhimili wa jitihada, nia/ari, motisha changamani, uwezo wa kufanikiwa na mwelekeo chanya. Utafiti ulifanyika mjini Kampala nchini, Uganda katika Ekedi ya Mukwano, Simlaw International Limited na soko la Kikuubo. Utafiti  ulijikita katika ujifunzaji na ufunzaji wa lugha ya pili na Isimujamii. Utafiti huu ulichanganua mikakati na mitindo ya kujifunza na kutumia lugha ya Kiswahili kibiashara pamoja na changamoto za ujifunzaji wa Kiswahili kama lugha ya biashara miongoni mwa wafanyabiashara jijini, Kampala. Usampulishaji dhamirifu ulitumiwa kwa kurejelea aina yake ya usampulishaji mpokezano  kifu  ambapo uteuzi dabwa dabwa ulitumiwa kuteuwa sampuli ya  wasailiwa 260 ya wafanyabiashara kutoka Ekedi ya Mukwano, Simlaw International Limited na soko la Kikuubo. Sampuli kusudio ilitumika kuteua Ekedi 2 na soko Moja  la biashara anuwai kuhusika katika utafiti huu. Mbinu za hojaji, usaili na uchuzaji zilitumiwa kukusanya data miongoni mwa wafanyabiashara nyanjani. Vifaa vya utafiti ni pamoja na hojaji, dodoso, mwongozo wa uchunzaji vilitumika kukusanya data nyanjani. Data ilichanganuliwa kutumia mkabala mseto na kuwasilishwa kimaelezo ukishirikisha majedwali. Matokeo ya utafiti yalionyesha kwamba wafanyabiashara walitumia mikakati ya nyimbo/ukariri, mwanafunzi kwa mwanafunzi, matumizi ya lugha chanzi, kuongea, mawasiliano, mitagusano ya ukuruba kati ya wanunuzi na wauzaji, teknolojia, mapango binafsi, utambuzi na urejeleaji. Mitindo ya mwingiliano iliyodhihirika ni dukuduku, kusikiza, ujifunzaji asilia, mwelekeo, hamasa, kuashiria na tabia za mjifunzaji. Hii ilifanyika kupitia kusikiza nyimbo, wafanyabiashara kufundishana wenyewe kwa wenyewe, uhamishaji sheria kutoka lugha chanzi, mawasiliano baina yao na wanunuzi, kutagusana na wajuao Kiswahili, matumizi ya teknolojia, kujipangia namna ya kujifunza, utambuzi, dukuduku, hamasa, mwelekeo, kuashiria na tabia ambazo baadhi ya wafanyabiashara walikuwa nazo. Utafiti huu ulibaini changamoto za kisarufi, muda wa kujifunza, kutumia lugha kimshitukizo, mwelekeo hasi, athari za kisiasa, umri, uoga, tofauti za kijinsia na kanuni za kiisimu. Utafiti huu utachangia katika taaluma ya Isimujamii na ujifunzaji wa lugha ya pili. Utafiti huu ulipendekeza tafiti zaidi kufanyika katika kutambua mikakati na mitindo zaidi katika sekta nyinginezo.
PhD Theses
</description>
<dc:date>2023-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5218">
<title>Uhakiki wa ubunilizi wa changamoto za ndoa katika riwaya teule za kiswahili kiuhusika na kiusimulizi</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5218</link>
<description>Uhakiki wa ubunilizi wa changamoto za ndoa katika riwaya teule za kiswahili kiuhusika na kiusimulizi
MBERESIA, Benard Tsimango
Ndoa ni asasi muhimu inayoiendeleza jamii na kudumisha uthabiti wake kupitia majukumu yake muhimu ya kuhakikisha wanajamii wapya wanazaliwa na kulelewa. Tafiti za kifasihi na za kisosholojia kuhusu ndoa zinaonyesha kuwa inaendelea kukosa uthabiti na kushindwa kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Tafiti za awali kuhusu ndoa katika fasihi ya Kiswahili zimebainisha changamoto zinazoiyumbisha na kufanya ishindwe kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Hata hivyo, tafiti hizi zimeegemea uchunguzi wa usawiri wa maudhui ya ndoa katika kazi mahususi za kifasihi.Kuna haja ya kuchunguza namna changamoto za ndoa zimejengwa kupitia vipengele vya kibunilizi kwa kurejelea kazi mbalimbali za kifasihi. Kwa msingi huu, utafiti huu unahakiki namna uhusika na usimulizi umetumika kujenga changamoto za ndoa  katika riwaya tofauti za Kiswahili zilizoandikwa na waandishi tofauti. Lengo la utafiti huu ni kuhakiki uhusika na usimulizi katika ubunilizi wa changamoto za ndoa katika riwaya teule za Kiswahili. Madhumuni ya utafiti huu ni; kueleza jinsi changamoto za ndoa zimesawiriwa kupitia usawiri wa wahusika katika riwaya teule za Kiswahili; kutathmini namna athari za changamoto za ndoa zimedhihirishwa kupitia usawiri wa wahusika katika riwaya teule za Kiswahili na hatimaye kufafanua namna njia za kukabiliana na changamoto za ndoa katika riwaya teule za Kiswahili zimewasilishwa kupitia mbinu za usimulizi. Utafiti huu unaongozwa na mseto wa nadharia ya umuundo- uamilifu kwa mujibu wa Merton (1957) na nadharia ya naratolojia kwa mujibu wa Genette (1980) na Kenan (1983). Muundo wa utafiti huu ni wa kiuchanganuzi. Eneo la utafiti huu ni la maktaba, muktadha wa fasihi na mahususi riwaya ya Kiswahili. Kundi lengwa ni riwaya za Kiswahili ambazo zimesawiri changamoto za ndoa. Usampulishaji dhamirifu uliwezesha kubainishwa kwa sampuli ya riwaya tano zifuatazo; Kiu (1972), Mwisho wa Kosa (1987), Maisha Kitendawili (2000), Ua la Faraja (2005) na Unaitwa Nani? (2008). Data ilikusanywa kutoka kwa riwaya teule kwa kutumia mbinu ya unukuzi kwa kutumia orodha ya uchunzaji. Data ilichanganuliwa kimaudhui na kuwasilishwa kimaelezo. Matokeo ya utafiti huu yanaonyesha kwamba changamoto za ndoa kama vile umaskini zimesawiriwa kupitia uhusika wao kimatendo, kiusemi, kimazingira na wa muonekano wa nje. Aidha yanaonyesha kuwa athari za changamoto za ndoa kama vile ukosefu au upungufu wa mahitaji ya kimsingi zimedhihirishwa na wahusika kupitia uhusika wao kimatendo, kiusemi, kimazingira na kwa muonekano wa nje. Hatimaye, matokeo haya yanaonyesha kuwa njia za kukabilia na changamoto za ndoa kama vile ushauri nasaha zimewasilishwa kupitia mbinu zifuatazo za usimulizi; usimulizi wa nafsi ya kwanza, usimulizi wa nafsi ya tatu, mtazamo wa ndani, mtazamo wa nje, msimulizi tawasifu, msimulizi wasifu na msimulizi horomo. Matokeo yanaonyesha tofauti na kulingana katika matumizi ya uhusika na usimulizi katika kujenga changamoto za ndoa kwenye riwaya teule. Utafiti huu unatarajiwa kuonyesha namna uumbaji wa wahusika na mbinu za usimulizi zinasawiri maudhui; unachangia utafiti zaidi kuhusu ndoa katika fasihi ya Kiswahili kwa kuhakiki ubunilizi wa changamoto zake na kupanua uelewa kuhusu changamoto hizi.
</description>
<dc:date>2021-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5211">
<title>Umilisi wa lugha ya kifasihi miongoni mwa wanafunzi wa shule za upili katika kaunti ndogo ya Wareng’</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/5211</link>
<description>Umilisi wa lugha ya kifasihi miongoni mwa wanafunzi wa shule za upili katika kaunti ndogo ya Wareng’
WAMBUA, Pauline Ndave
Umilisi wa lugha ya kifasihi kutokana na fasihi andishi ya Kiswahili ni uti wa mgongo kwa ufanisi wa mtihani wa Kiswahili. Wanafunzi wanapoanza kidato cha kwanza huwa wamepata alama nzuri katika mtihani wa Kiswahili. Mtaala na mtihani katika hiki kiwango hauhusishi umilisi wa lugha ya kifasihi kutokana na vitabu vya fasihi andishi vilivyoteuliwa. Kwa hivyo, wanafunzi huanza kidato cha kwanza kabla hawajatangulizwa katika umilisi wa lugha ya kifasihi unaotokana na fasihi andishi. Ukosefu wa utangulizi wa lugha ya kifasihi kabla ya kujiunga na kidato cha kwanza huzua pengo la umilisi wa lugha ya kifasihi. Hii ni kwa sababu punde baada ya kujiunga na shule za upili,  wanafunzi wa kidato cha pili hutahiniwa katika vipengee vya lugha ya kifasihi, ambapo hawana umilisi wa lugha ya kifasihi wa kukabiliana na hiyo mitihani. Hali hii huzua msingi dhaifu wa kuipasi mitihani ya kieneo na  kitaifa katika kidato cha nne. Ufanisi wa matokeo ya mitihani kabla ya kuhusishwa na lugha ya kifasihi, na udhaifu wa matokeo baada ya kidato cha kwanza, ni hali iliyochochea na kufungua mwanya wa swala la utafiti huu, ambao ulichunguza umilisi wa lugha ya kifasihi miongoni mwa wanafunzi wa shule za upili  katika kaunti ndogo ya Wareng’, kaunti ya Uasin Gishu. Madhumuni ya utafiti ni: Kuchunguza vigezo vya umilisi wa lugha ya kifasihi vya fasihi andishi ya Kiswahili ambavyo wanafunzi wanao hitimu kidato cha pili wanavitumia ili kutatua tatizo la pengo la umilisi wa lugha hiyo. Kupambanua mikakati ya kiuamalifu na kimakusudi ambayo wanafunzi kufikia kidato cha pili wameitumia ili waweze kusoma vitabu vya fasihi andishi ya Kiswahili vilivyoteuliwa na Taasisi ya kukuza Mitaala Nchini. Kudadavua mfanano na tofauti za umilisi wa lugha ya kifasihi kati ya wanafunzi wa kidato cha nne na  kidato cha pili kiulinganishi. Kubainisha iwapo kufikia kidato cha nne wanafunzi walihusishwa na mikakati ya mtaala shirikishi nje ya mtaala rasmi ili kukuza umilisi wa lugha ya kifasihi. Nadharia ya Uamalifu, iliyoasisiwa na John Dewey (1952) na kuendelezwa baadaye na Tomasello (20000) ilitumiwa. Mihimili iliyouongoza utafiti ni: Mwanafasihi huhitaji umahiri wa kufafanua maana za dhana za kiusomi katika matumizi ya kila siku; wazo na maelezo ya kiusomi yaonyeshwe kwa njia ya utendaji; Umilisi wa lugha sio tukio funge la wakati mmoja; Umilisi wa lugha unaweza kupatikana nje ya darasa rasmi. Nadharia hii iliongoza utafiti kubainisha kwamba stadi za lugha zinaweza kutumiwa  kiuamalifu ili kuibua umilisi wa kinachosomwa kwa ufanisi mkuu. Muundo wa utafiti wa kisifa ulizingatiwa. Utafiti uliendelezwa katika kaunti ndogo ya Wareng’.  Kithematiki utafiti ulijikita katika matumizi ya lugha ya kifasihi katika fasihi andishi kwa wanafunzi wa sekondari. Kundi lengwa lilikuwa wanafunzi wa kidato cha pili na kidato cha nne wanaofanya mitihani ya Kiswahili Wareng’, ambao walikuwa jumla ya 3873. Usampulishaji ulihusisha: Shule 12 za kiwango cha Kaunti ndogo; walimu 12 wa Kiswahili; na mtaalamu mmoja mmoja kutoka Taasisi ya Kukuza Mitaala Nchini na Baraza la Mitihani la Kitaifa la Kenya. Idadi ya shule 12  ilisampulishwa kinasibu kama thuluthi moja ya shule zote 38 zilizokuwa zimesajiliwa. Kati ya kundi lengwa ya 3873 kutoka kidato cha nne na cha pili, sampuli ilikuwa 2073 kutoka kidato cha pili na 1800 kutoka kidato cha nne. 2073 ilipimwa kwa asilimia 11% ili kupata sampuli ya 230; 1800 ilipimwa vivyo hivyo kwa mujibu wa wataalamu na kupata sampuli ya 200. Mbinu za kukusanya data zilikuwa uchunzaji darasani, usaili, upekuzi, dodoso na hojaji. Vifaa vilivyotumiwa ni mwongozo wa orodha ya uchunzaji, hojaji, maktaba  na matini za kifasihi. Data ilichanganuliwa na kuwasilishwa kiwingi idadi na kisifa. Utafiti  uliwekwa katika sura tano. Matokeo yalionyesha kwamba wanafunzi wa shule za upili katika kaunti ndogo ya Wareng’ wana kiwango cha chini cha umilisi wa lugha ya kifasihi, kwa hivyo walihitaji kuhusishwa katika kuisoma fasihi andishi ili wapate umilisi wa lugha ya kifasihi kwa manufaa ya ufanisi. Umuhimu wa utafiti huu ni pamoja na kuonyehsa ubora wa kuwahusisha wanafunzi wa shule za upili katika umilisi wa lugha ya kifasihi kama kiungo muhimu kwa ufanisi; kuongezea maarifa ya kiusomi, na kuonyesha nafasi ya stadi za lugha katika kujenga umilisi wa lugha ya kifasihi.
</description>
<dc:date>2021-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1127">
<title>Mwingiliano matini wa maumbo ya fasihi simulizi ya Kiafrika na matini teule za Biblia</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1127</link>
<description>Mwingiliano matini wa maumbo ya fasihi simulizi ya Kiafrika na matini teule za Biblia
AGISO, Yunia  Otieno
Biblia takatifu inayo misingi yake mikuu katika tamaduni za Wayahudi, yaani ni mkusanyiko wa vitabu vyenye maumbo ya fasihi simulizi. Ingawa kumekuwa na tafiti anuai kuhusu maumbo ya fasihi simulizi, chache zimefanywa kuhusu mwingiliano matini wa maumbo ya fasihi simulizi katika Biblia. Utafiti huu ulidhamiria kutathmini maumbo ya fasihi simulizi katika vitabu teule vya Biblia ili kuziba hili pengo. Utafiti huu ulilenga kuhakiki mwingiliano matini kati ya fasihi simulizi na Biblia. Madhumuni ya utafiti huu yalikuwa: kuchanganua maumbo ya fasihi simulizi katika matini teule katika Biblia; kupambanua mwingiliano matini wa fasihi simulizi na matini teule ya Biblia; kutathmini mchango wa Biblia katika ukuzaji wa fasihi simulizi. Upeo wa utafiti huu ni maumbo ya fasihi simulizi katika vitabu saba vya Biblia ya Tafsiri Jipya la Kimataifa; kitabu cha Mwanzo, Wafalme wa kwanza na Wafalme wa pili, Zaburi, Mithali, Mathayo na Luka. Nadharia iliyoongoza utafiti huu ni nadharia ya mwingiliano matini iliyoasisiwa na Julia Kristeva mwaka wa 1969. Mihimili mitatu ya nadharia hii ni; kazi za kifasihi huingiliana na kuhusiana; matini hupeana umatini ambamo matini nyingine zinaweza kuundwa na kufasiriwa; fasihi hutokana na fasihi. Muundo wa kimaelezo ulizingatiwa. Ili kupata sampuli yenye sifa zifaazo, usampulishaji dhamirifu ulitumiwa. Data ilikusanywa maktabani kwa kusoma na kudondoa maumbo ya fasihi simulizi yaliyoafiki madhumuni ya utafiti kwa kutumia orodha ya uchunzaji. Uchanganuzi wa yaliyomo ulifanywa. Data iliwasilishwa kwa njia ya maelezo nayo matokeo yakafasiriwa kuzingatia swala la utafiti, mihimili ya nadharia na madhumuni ya utafiti. Matokeo ya utafiti huu yalikuwa ifuatavyo; kwanza, maumbo manne makuu ya fasihi simulizi yalidhihirika katika vitabu vilivyoteuliwa; pili, ilibainika kwamba fasihi simulizi huingiliana na matini teule ya Biblia; tatu, Biblia ina mchango mkubwa katika fasihi simulizi hivyo husaidia katika ukuzaji na uhifadhi wake. Utafiti ulihitimisha kuwa kuna mwingiliano matini kati ya fasihi simulizi na matini teule za Biblia. Mwingiliano huu ulidhihirika kutokana na jinsi maumbo ya fasihi simulizi yalivyoingiliana na matini teule za Biblia. Utafiti unatarajiwa kupanua uwanja wa fasihi simulizi kwa kukuza swala la mwingiliano matini. Utafiti unapendekeza kuwa Biblia itumiwe kama rejea ya maumbo ya fasihi simulizi. Hii itachochea wasomi wa fasihi simulizi na watafiti wa baadaye kusoma Biblia kama kitabu cha fasihi simulizi, hasa wanapochanganua maumbo ya fasihi simulizi.
Masters' Thesis
</description>
<dc:date>2017-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1125">
<title>Uchanganuzi wa kileksikografia wa hiponimia za leksimu nomino na vitenzi vya kiswahili na tafsiri zake katika kiluo</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1125</link>
<description>Uchanganuzi wa kileksikografia wa hiponimia za leksimu nomino na vitenzi vya kiswahili na tafsiri zake katika kiluo
OKAL, Benard Odoyo
Ingawa hiponimia hudhihirika miongoni mwa kategoria mbalimbali za maneno, tafiti za Kiswahili zimeelekea kushughulikia hiponimia za nomino na kupuuza kategoria nyingine kama vile vitenzi, vielezi na vivumishi. Tafiti hizi zimefanywa pia bila kuhusisha mitazamo ya kiisimu ya uainishaji na nadharia faafu zingativu. Aidha, hakuna tafiti za kimuundo na kimtindo kuhusu hiponimia zilizofanywa baina ya Kiswahili na lugha nyingine za Kiafrika. Hivyo basi, utafiti huu ulihusisha uchanganuzi wa kileksikografia wa hiponimia za leksimu nomino na vitenzi vya Kiswahili na tafsiri zake katika Kiluo kwa minajili ya kuimarisha tafiti zao linganishi za kimuundo na kimtindo. Madhumuni yafuatayo yalizingatiwa: kuchanganua kileksikografia na kuainisha hiponimia za leksimu nomino na vitenzi vya Kiswahili, kutafsiri kiisimu hiponimia za nomino na vitenzi vya Kiswahili katika Kiluo, na kulinganisha na kulinganua kimuundo na kimtindo hiponimia za nomino na vitenzi vya Kiswahili na Kiluo. Utafiti huu uliongozwa na mseto wa nadharia ya uchanganuzi vijenzi ya Katz na Fodor ya kuchanganua vijenzi vya maana kileksika kwa kuzingatia sifa bainifu iliyotumiwa kuainisha hiponimia za Kiswahili, na nadharia ya tafsiri kwa mujibu wa Catford iliyotumiwa kutafsiri hiponimia za Kiswahili katika Kiluo. Utafiti huu ulihusisha uchanganuzi wa hiponimia za nomino na vitenzi vya Kiswahili kutoka KK21 na KKS na visawe vyake katika Kiluo kutoka EDD na DED. Muundo kimaelezo unaohusisha maelezo na uchanganuzi data katika majedwali ya solo ulizingatiwa. Utafiti huu ulifanyika maktabani na nyanjani katika kaunti ndogo ya Kisumu Mashariki. Usampulishaji dhamirifu ulitumiwa kuteua wasailiwa Waluo 35, na pia hipanimu kuu 28 za nomino na 24 za vitenzi zilizochanganuliwa hadi kufikia kiwango kifu. Mbinu za upekuzi na usaili muundo usorasmi zilitumiwa kukusanya data huku modeli ya uhusiano wa leksikoni kisintaksia na dodoso zikitumiwa kama vifaa. Data husika ziliyakinishwa kwa kutumia mtindo wa uthibitishwaji, kuchanganuliwa kimaudhui na katika majedwali ya solo, na hatimaye kuwasilishwa kileksikografia. Utafiti huu ulibainisha kuwa hiponimia za leksimu za Kiswahili huweza kuchanganuliwa kileksikografia na kuainishwa kimaudhui katika mikondo sita kama vile kitambuzi, kidhanishi au kiuamilifu, kijiografia, kitukio, kihali na kitendo.Visawe linganifu na kapa hudhihirika katika tafsiri ya hiponimia za Kiswahili katika Kiluo. Miundo na mitindo ya hiponimia hulingana na kutofautiana katika uchanganuzi wa hiponimia kiuamilifu kwa sababu ya tofauti za kijiografia na kitamaduni za lugha hizi mbili. Matokeo yake ni mchango mkubwa katika taaluma za semantiki kileksika na tafsiri, mafunzo ya misamiati ya Kiswahili na Kiluo, na kudhukuriwa kama makala kivo ya leksikografia thaniya ya Kiswahili na Kiluo, na kama matini ya thesauri sahili iliyotafsiriwa ya lugha hizi mbili.
Phd Thesis
</description>
<dc:date>2018-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
<item rdf:about="https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1114">
<title>Uchanganuzi wa uwasilishaji wa kifo katika mashairi teule ya Kiswahili</title>
<link>https://repository.maseno.ac.ke/handle/123456789/1114</link>
<description>Uchanganuzi wa uwasilishaji wa kifo katika mashairi teule ya Kiswahili
ODONGO, Fredrick Orinda
Kifo ni swala zito na linaloibua hisia zaidi. Uwasilishaji wa dhana ya kifo katika tanzu anuwai za fasihi huwa kwa namna tofauti. Katika ushairi kifo huibuliwa kwa lugha ya pekee yenye mnato wa hisia na mashiko zaidi. Ushairi hutumia lugha ya mkato na mapigo ya sauti yanayovutia na kunata pindi yanapowasilishwa kupitia kughani, usomaji na ukariri. Uchambuzi mwingi wa dhana ya kifo katika ushairi wa Kiswahili uliwahi kufanywa katika ushairi mbolezi ambao ni wa kisimulizi lakini swala hili katika ushairi andishi hutajwa tu kwa ufinyu wala haushughulikiwi kwa kina. Utafiti huu ulichambua uwasilishaji wa kifo katika mashairi teule ya Kiswahili.  Uchambuzi huu ulifanywa kwa malengo ya; kutambua na kueleza taswira ya kifo; kubainisha visababishi vya kifo; na kuchunguza utata unaojitokeza katika ufafanuzi wa dhana ya kifo kama wanavyodhihirisha wasanii katika mashairi teule ya Kiswahili. Malengo haya yalifikiwa kwa kuzingatia mashairi matatu teule; Inkishafi, Mwana Kupona na ‘Usiniuwe’ katika diwani ya Sauti ya Dhiki. Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya uhalisia kama ilivyofafanuliwa na Georg Lukacs (1938). Mihimili ya nadharia hii iliyotumika ni pamoja na tajriba ya mwandishi, historia ya jamii, muundo wa kazi, vielelezo na lugha. Utafiti ulikuwa wa kimaktaba. Mtafiti aliteua matini tatu za ushairi wa Kiswahili na kujikita maktabani na kuzichambua kwa kina huku akirejelea malengo ya utafiti. Uteuzi ulifanywa kimaksudi kwa kuzingatia usawirishaji wa dhana ya kifo. Muundo wa uwasilishaji data ulikuwa wa kimaelezo. Kupitia mihimili ya nadharia ya uhalisia, utafiti huu ulibaini kuwa; taswira ya kifo kulingana na mashairi teule ni pamoja na dhoruba ya kifo, kifo kinatamausha, uchungu wa mauti, kifo ni hatima ya kila kiumbe, kifo kina upweke, kifo si mwisho wa maisha na kifo kina ukatili. Usawiri wa kifo pia hujikita katika mazingira ya mtunzi ambayo hujitokeza katika vipengee vya wakati, dini au utamaduni na lugha. Aidha, kifo ni kitu kilicho na chanzo chake ikiwa ni Mungu, shetani na mtu. Utafiti huu ulidhihirisha kuwa hakuna mpaka bayana baina ya kifo na uhai hivyo mwanadamu anajikuta katika mkanganyiko wa kuishi huru duniani kwa hofu ya yatakayompata akhera. Utata huu hujitokeza katika kuelewa mwanzo na mwisho wa maisha, maisha baada ya kifo na uwezo wa kuzungumza na Mungu katika ufu. Utafiti huu ulihitimisha kuwa kifo ni hatima ya kila kiumbe na ni vema mwanadamu kukikubali na kuwa radhi nacho kwani huletwa na nguvu za kimaumbile nje ya uwezo wake. Akiishi mwanadamu, huwa yu mbioni akingoja kifo na ahera kwa kutegemea alivyoishi duniani. Ni mapendekezo ya utafiti huu kuwa kifo ni kiungo cha maisha kinachofanya uhai kuthaminiwa zaidi. Uwepo wa kifo hupatia maisha maana na ukosefu wake huyafanya kukosa kufasiriwa. Kutokana na utata wa dhana ya kifo, ni muhimu utafiti zaidi ufanyike kwa kuzingatia dhana ya uhai ili kuweka mwangaza zaidi kuhusu mpaka baina ya kifo na uhai na chanzo cha kifo; na utafiti linganishi ufanywe ili kubainisha taswira ya kifo katika tanzu nyinginezo za fasihi.
Masters' Thesis
</description>
<dc:date>2014-01-01T00:00:00Z</dc:date>
</item>
</rdf:RDF>
